Kamati ya Ushauri ya Wilaya ya Pangani (DCC) imepitisha mapendekezo ya rasimu ya Mpango na Bajeti yenye thamani ya Shilingi bilioni 23.4 kwa mwaka wa fedha 2026/27.
Akizungumza katika kikao cha kamati hiyo kilichofanyika leo, tarehe 12 Februari 2026, katika ukumbi wa YMCA, Kaimu Mkuu wa Wilaya ya Pangani, Mhe. Ayubu Sebabili, amesema ni muhimu rasimu ya Mpango na Bajeti izingatie vipaumbele vya Serikali, ikiwemo kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.

Ameongeza kuwa Serikali tayari imetangaza kuanza utekelezaji wa mpango wa Bima ya Afya kwa Wote, hivyo ni wajibu wa viongozi na watendaji kuhakikisha wananchi wanaelewa umuhimu wa mpango huo ili wawe na uhakika wa kupata huduma za afya wanapozihitaji.

Aidha, amesisitiza umuhimu wa kufanya tathmini ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ili kubaini kama inatekelezwa kwa kuzingatia thamani halisi ya fedha, sambamba na kudumisha nidhamu ya matumizi ya fedha za umma.
Kwa upande wake, Mkuu wa Idara ya Mipango na Uratibu, Ndugu Semeon Vedastus, ametaja baadhi ya vipaumbele vitakavyotekelezwa kwa kutumia mapato ya ndani kuwa ni pamoja na kutenga fedha kwa ajili ya mikopo ya asilimia 10 kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, utekelezaji wa afua za lishe, ujenzi wa miundombinu ya shule pamoja na kuboresha miundombinu ya mifugo.
Pangani District Council
Sanduku la Posta: 89 Pangani -Tanga
Namba ya Mezani: +255 (0) 27 2630058
Namba ya simu: 0658100588/062289307
Barua Pepe : ded@panganidc.go.tz
Hakimiliki @ 2017 Halmashauri ya Wilaya Pangani .Haki Zote Zimehifadhiwa