Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe .Balozi. Dkt. Bashiru Ally Kakurwa (Mb) leo tarehe 19 Februari 2026 amefanya ziara ya kikazi Wilayani Pangani katika shamba la utafiti wa magonjwa ya mifugo kwa lengo la kuhakiki mipaka ya shamba la wizara ya mifugo dhidi ya wafugaji waliovamia sehemu ya eneo hilo.

Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Waziri amezungumzia kwa kina suala la migogoro ya ardhi na uvamizi wa maeneo ya malisho, akisisitiza umuhimu wa kulinda na kusimamia ipasavyo rasilimali ardhi ili kuimarisha amani na tija katika shughuli za ufugaji.

Amesema Serikali imeandaa mipango madhubuti ya usimamizi wa maeneo ya malisho ili kuhakikisha wafugaji wanapata mazingira bora ya uzalishaji.
Aidha, amefanya ukaguzi wa maeneo ya malisho na miundombinu ya shamba, akielekeza maboresho ya haraka ili kuongeza ubora wa huduma na uzalishaji.

Mheshimiwa Waziri pia amesisitiza kuwa shamba hilo liendelezwe kuwa kituo maalum cha ulihimilishaji na uzalishaji wa mbegu bora za mifugo, hatua itakayosaidia kuongeza tija, ubora wa mifugo na kipato kwa wafugaji wa Pangani na maeneo jirani.
Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuendeleza sekta ya mifugo kwa vitendo, kusikiliza wananchi, na kuhakikisha rasilimali za mifugo zinatumika kwa ufanisi kwa manufaa ya jamii na Taifa kwa ujumla.
Pangani District Council
Sanduku la Posta: 89 Pangani -Tanga
Namba ya Mezani: +255 (0) 27 2630058
Namba ya simu: 0658100588/062289307
Barua Pepe : ded@panganidc.go.tz
Hakimiliki @ 2017 Halmashauri ya Wilaya Pangani .Haki Zote Zimehifadhiwa